Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC) imeamua kuondoa kikosi cha kulinda amani kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) kufuatia mashambulizi ya kasi ya waasi wa M23 ambayo yalisababisha vifo vya walinda amani.
Viongozi wa SADC walifikia uamuzi huo katika mkutano wa dharura uliofanyika kwa njia ya mtandao siku ya Alhamisi, kujadili hali mbaya ya usalama na kibinadamu mashariki mwa DRC.
Angalau wanajeshi 20 kutoka Afrika Kusini, Tanzania, na Malawi waliuawa wakati waasi wa M23 walipouteka mji wa Goma, mashariki mwa DRC, mnamo Januari.
Ujumbe wa SADC nchini DRC (SAMIDRC) ulianza kutumwa tarehe 15 Desemba 2023, na mamlaka yake yalirefushwa tu mnamo Novemba mwaka jana.
Katika tamko lao, viongozi wa kikanda walitoa wito wa suluhisho la “kidiplomasia na kisiasa” kwa mzozo huo ambao umewafanya mamilioni ya watu kuwa wakimbizi.
“Summit imesitisha mamlaka ya SAMIDRC na kuelekeza kuanza kwa kuondolewa kwa hatua kwa hatua kwa wanajeshi wa SAMIDRC kutoka DRC,” inasema sehemu ya tamko hilo.