Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Doto Biteko ametaja vipaumbele vya Wizara ya Nishati katika Bajeti ya mwaka wa fedha 2025/2026 ikiwemo kuendelea kutekeleza miradi ya uzalishaji, usafirishaji, usambazaji umeme na kufikisha gridi ya Taifa katika Mikoa iliyosalia ya Rukwa, Kagera, Lindi na Mtwara;
Akiwasilisha vipaumbele hivyo kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, jijini Dodoma, Dkt. Biteko amesema vipaumbele hivyo vimezingatia mpango wa Taifa wa Nishati wa mwaka 2025 hadi 2030.
“Mhe. Mwenyekiti vipaumbele hivi vimezingatia mpango wa Taifa wa Nishati wa mwaka 2025-2030 (National Energy Compact 2025-2030) utakaosaidia upatikanaji na uunganishaji wa umeme kwa wananchi, kuongeza mchango wa nishati jadidifu katika uzalishaji wa umeme na ushiriki wa Sekta Binafsi katika maendeleo ya Sekta ya Nishati”. Amesema Dkt. Biteko
Katika hatua nyingine, Dkt. Biteko amesema Serikali imewajengea wazawa uwezo mkubwa wa kutekeleza miradi ya umeme huku akitolea mfano wa ajira kwenye miradi ya umeme kufikia idadi ya 53,000,
Amesema Dunia inahitaji nishati na mahitaji ya umeme yamekuwa yakiongezeka kwa kasi hivyo Serikali itaendelea kuongeza vyanzo vya kuzalisha umeme ili kukidhi mahitaji ya Watanzania.
Awali, Mkurugenzi wa Sera na Mipango, Wizara ya Nishati, Petro Lyatuu alisema kuwa katika kuhakikisha kunakuwa na upatikanaji wa umeme wa uhakika Wizara itaendelea kuimarisha Gridi ya Taifa (National Grid Stabilization Project) pamoja na kufanya matengenezo na ukarabati wa mitambo ya kuzalisha umeme;